Dar es Salaam-Wakinamama waliolazwa katika wodi ya wanawake ya Hospitali ya Sinza jijini Dar es Salaam wamepatiwa msaada wa Comfy Mum pants uliotolewa na kampuni ya Comfy Mum kwa kushirikiana na Chemba ya Taifa ya Biashara (TNCC), ikiwa ni sehemu ya kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani na kuonyesha upendo na kujali afya ya wanawake katika jamii.
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mkurugenzi wa Comfy Mum, Bi. Irene Mville alisema kampuni hiyo imeona umuhimu wa kushiriki katika kuunga mkono wanawake, hususan waliotoka kujifungua na wanaokabiliwa na changamoto ya hedhi nyingi.
“Katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Comfy Mum tumeona ni vyema kuwafikia wanawake waliopo hospitalini na kuwapatia mahitaji haya muhimu ili kuwafariji na kuwapa faraja katika kipindi hiki,” alisema Bi. Mville.
Kwa upande wake, Afisa Rasilimali Watu wa TNCC, Bi. Judith Sarakikya, alisema ushirikiano huo unaonyesha dhamira ya sekta binafsi kushiriki katika kuimarisha ustawi wa wanawake.
“TNCC tunaamini kuwa kumwezesha mwanamke kunahusisha pia kujali afya na ustawi wake, ushirikiano huu na Comfy Mum unaonyesha namna sekta binafsi inavyoweza kushiriki kusaidia jamii,” alisema Sarakikya.
Naye Afisa Muuguzi Mfawidhi wa Hospitali ya Sinza, Bi. Judith Katemba, aliishukuru Comfy Mum na TNCC kwa msaada huo akisema utasaidia kuwafariji wagonjwa waliolazwa hospitalini.
“Tunawashukuru sana Comfy Mum na TNCC kwa kutukumbuka. Msaada huu ni muhimu kwa wagonjwa wetu na unaonyesha kuwa jamii inaendelea kuwajali wanawake hata wanapokuwa kwenye changamoto za kiafya,” alisema Katemba.
Aliongeza kuwa hatua hiyo inaakisi mshikamano wa kijamii na kuthibitisha umuhimu wa ushirikiano katika kuunga mkono wanawake hususan katika kipindi hiki cha kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

