Waziri wa maji Mhe. Jumaa Hamidu Aweso amesema Wizara ya maji imepiga hatua kwenye ujenzi wa miradi ya maji nchini hivyo kinachotakiwa kwa sasa ni kuboresha huduma kwa wateja na kudhibiti upotevu wa maji.
Mhe. Waziri Aweso amesema hayo wakati akizungumza kwenye kikao kazi cha wakurugenzi wa huduma kwa wateja wa mamlaka za maji nchini kilichofanyika Mei 28, 2025 jijini Mbeya, kikao kinachofanyika kwa muda wa siku tano kuanzia Mei 26, 2025.
Amemuagiza katibu mkuu wa wizara hiyo Mhandisi Mwajuma Waziri, kuelekeza nguvu zake kwenye kuwasimamia watendaji kuhakikisha huduma ya maji inakuwa bora kwa wateja wao kwani kwa sasa miradi imeendelea kujengwa kila uchao bila udanganyifu tofauti na hapo awali.
Pia Waziri Aweso ameeleza kukerwa na kitendo cha wateja wapya kukaa muda mrefu wa hadi miezi sita wakisubiri kuunganishiwa huduma ya maji akikemea suala hilo kwa wataalam wa maji kote nchini na kuacha tabia ya kukadiria bill za maji wateja bila kuwa na uhakika nazo hivyo kuwaumiza wananchi.
Kwa upande wake Katibu mkuu wa wizara ya maji Mwajuma Waziri amesema wakati muafaka kwenda kuthibitisha kwa vitendo kauli mbiu ya matarajio ya wateja kwa kuhakikisha huduma inakuwa bora zaidi.
Hata hivyo amewataka wataalam hao kujenga ushirikiano ili kuboresha utendaji kazi kwenye idara na mamlaka zote za maji nchini.
Mkurugenzi msaidizi wa usimamizi utoaji wa huduma kutoka wizara ya maji bi. Nancy Mduma, amesema baadhi ya changamoto zinazozikabili idara ya maji ni madeni ikiwemo kwenye baadhi ya taasisi za umma na kuahidi kuendelea kulivalia njuga suala la madeni ikiwa ni pamoja na uboreshaji huduma kwa wateja kupitia pia mafunzo.
Kikao hicho kilianza Mei 26, 2025 na kunatarajiwa kutamatika Mei 30, 2025 kikijumuisha wakurugenzi wote wa huduma kwa wateja kote nchini na wataalam mbalimbali wa wizara ya maji.