Benki ya Equity Tanzania kwa kushirikiana na kampuni ya Mastercard imezindua kadi mpya mbili za malipo – Mastercard Gold Debit na Mastercard World Debit – katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 4 Juni 2025.
Uzinduzi huo umefanyika kwa na Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Maryprisca Mahundi.
Akizungumza katika hafla hiyo, mhandisi Mahundi amesema kadi hizo ni sehemu ya mageuzi ya kidijitali na ujumuishwaji wa kifedha yanayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.
Amesisitiza kuwa huduma hizo mpya zitawawezesha Watanzania kupata huduma za kifedha salama, za kisasa, na zenye uwazi, hivyo kuongeza ushiriki wao katika uchumi wa kidunia.
Kadi hizo zitatumika kimataifa, zikiwa na faida kama upatikanaji wa huduma kwenye zaidi ya viwanja vya ndege 1,000, bima ya usafiri, huduma za hoteli, ulinzi wa miamala na ofa kutoka kwa chapa kubwa za kimataifa. Aidha, kadi hizo zitawawezesha Watanzania, wakiwemo wafanyabiashara, wanafunzi na wasafiri wa kimataifa, kufanya miamala kwa urahisi na usalama zaidi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Equity Tanzania, Bi. Isabela Maganga, amesema benki hiyo inaendelea kujikita katika ubunifu wa bidhaa zinazokidhi mahitaji ya kila kundi la mteja.
Ameeleza kuwa benki hiyo ina matawi zaidi ya 17 na mawakala zaidi ya 3,000 nchi nzima, hivyo kuwawezesha wananchi wa maeneo ya mijini na vijijini kunufaika na huduma bora za kifedha.
Naibu Waziri ameitaka jamii kutumia huduma za kibenki za kidijitali badala ya kutegemea pesa taslimu, akisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ni msingi wa kujenga uchumi jumuishi.
Amehitimisha kwa kuipongeza
Equity na Mastercard kwa mchango wao mkubwa katika kukuza maendeleo ya kiuchumi kupitia mifumo ya kisasa ya kifedha.