Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprsca Mahundi, amewatoa hofu wananchi kuwa Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa wananchi wote wanapata huduma bora za mawasiliano hasa maeneo ya vijijini.
Katika kutekeleza hilo, kata ya Mkwamba iliyopo mkoani Rukwa yenye jumla ya vijiji vinne—Swaila, Tambaruka, Itindi na Lyele—imepata mafanikio makubwa kupitia miradi ya Serikali inayolenga kuboresha mawasiliano.
Kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), Serikali imefanikiwa kujenga minara ya mawasiliano kwa kushirikiana na makampuni ya mawasiliano ya VODACOM na HALOTEL.
Mnara wa Vodacom umejengwa katika Kijiji cha Tambaruka kupitia mradi wa Tanzania ya Kidijitali (DTP), huku mnara wa Halotel ukijengwa katika Kijiji cha Itindi chini ya awamu ya tatu ya mradi wa mawasiliano vijijini.
Minara yote imewashwa na inatoa huduma kwa wananchi, hatua inayowezesha kuimarika kwa shughuli za kijamii na kiuchumi kupitia mawasiliano ya uhakika.
Meneja wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) Mkoa wa Rukwa, Bw. Ching’uli, amesema utekelezaji wa miradi ya UCSAF umeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya wananchi wa Wilaya ya Nkasi kwa kuwaunganisha na huduma muhimu za mawasiliano.
Amesema kuwa kupitia minara iliyojengwa katika maeneo kama Kala, Izinga na Mlambo, wananchi wameweza kuwasiliana kwa urahisi zaidi, kupata taarifa kwa haraka, pamoja na kuendesha shughuli zao za biashara na kijamii kwa ufanisi.
“Huduma hizi zimefungua dunia kwa wananchi waliokuwa hawajawahi kupata mawasiliano kabisa,” alisema Ching’uli.
Aidha, Bw. Ching’uli ameongeza kuwa TTCL kama mtoa huduma wa ndani inaendelea kushirikiana na serikali katika kuhakikisha huduma zinafika hadi maeneo ya pembezoni ambayo bado hayajafikiwa.
Amesema kuwa pamoja na changamoto za miundombinu na jiografia ya maeneo mengi ya Nkasi, shirika lao limejipanga kuhakikisha kuwa kila mnara unaojengwa unatoa huduma bora na za uhakika kwa wananchi.
Aliwataka wananchi kutumia miundombinu hiyo kwa tija ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika jamii zao.
Nae Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Makongolo Nyerere ametumia wasaa huo kuishukuru serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote UCSAF kwa kupeleka huduma ya mawasiliano katika mkoa huo.