Browsing: Video Mpya

ZAIDI ya kaya 200 zimepata madhara ya kukosa makazi baada ya nyumba zao kuezuliwa na nyingine kubomoka kufuatia mvua kubwa zilizoambatana na upepo mkali zinazoendelea kunyesha katika Nyanda za Juu Kusini.

Mbali na makazi kuharibika, vyakula na mavazi pia vimeathirika baada ya maji kujaa kwenye nyumba na mali nyingi kufunikwa na tope.

Uharibifu huo umeripotiwa katika kata sita, ambazo ni Iganzo, Isanga, Karobe, Iyunga, Nzovwe na Iwambi, wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Patrick Mwalunenge, aliyefika kujionea hali halisi ya wananchi walioathirika.

Baadhi ya wakazi wamesema chanzo kikubwa cha mafuriko hayo ni mifereji kuziba, hali iliyosababisha maji kuingia moja kwa moja kwenye makazi yao.

Licha ya uharibifu mkubwa wa mali na makazi, hakuna madhara ya kibinadamu yaliyoripotiwa hadi sasa.

Meneja Uhamasishaji Uwekezaji kutoka TISEZA, Daudi Riganda, amesema mamlaka hiyo inaendelea kuhamasisha uwekezaji ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za biashara nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutembelea mradi wa Babito Trading Company katika Mbeya, alisema uwekezaji huo unaomilikiwa kwa asilimia 100 na Watanzania umegharimu zaidi ya shilingi bilioni nane.

Alisema mradi huo ni chanzo cha mapato kwa jiji la Mbeya na pia kwa TRA, huku ukiwa mfano wa mafanikio ya uwekezaji wa ndani kutokana na mazingira mazuri ya biashara yaliyopo Tanzania.

Aidha, alibainisha kuwa motisha za uwekezaji, ikiwemo punguzo la kodi na unafuu wa ushuru kwa baadhi ya vifaa vilivyoagizwa kutoka China, zimechangia kupunguza gharama za mradi.

KANISA LA MORAVIAN TANZANIA LATOA TUZO MAALUM KWA YONA SONELO BAADA YA KUTUNUKIWA SHAHADA YA HESHIMA AUSTRALIA

Kanisa la Moravian Tanzania (KMT) limetoa tuzo maalum kwa muumini wake na mfanyabiashara maarufu nchini, Yona Sonelo, kufuatia kutunukiwa Shahada ya Heshima na Chuo Kikuu cha Australia kutokana na mchango wake mkubwa kwa jamii.

Hafla ya kukabidhi tuzo hiyo imefanyika mkoani Tabora, ambapo viongozi wa kanisa, waumini pamoja na wadau mbalimbali walihudhuria kushuhudia tukio hilo muhimu.

Akizungumza katika hafla hiyo, viongozi wa Kanisa la Moravian Tanzania wamesema kuwa Sonelo amekuwa mfano wa kuigwa kwa kuunganisha imani na vitendo kupitia shughuli zake za kibiashara na kijamii, ikiwemo kusaidia makundi yenye uhitaji na kuchangia maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake, Yona Sonelo amelishukuru kanisa kwa kutambua juhudi zake, akisema mafanikio aliyoyapata ni matokeo ya imani, ushirikiano na msaada kutoka kwa familia, kanisa na jamii kwa ujumla.

Tuzo hiyo ni ishara ya kuthamini mchango wake endelevu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku ikiwahamasisha waumini na Watanzania kwa ujumla kuendelea kufanya kazi kwa bidii na uadilifu.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Region, Beno Malisa, amesema Serikali ipo tayari kutoa ushirikiano kwa wawekezaji wote wanaotaka kuwekeza mkoani humo ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi.

Amesema hayo wakati wa uzinduzi wa tawi la Strategies Insurance, kampuni inayotoa huduma za bima, uliofanyika jijini Mbeya. Amepongeza uamuzi wa kampuni hiyo kufungua tawi katika mkoa huo, akieleza kuwa hatua hiyo itarahisisha upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi na wafanyabiashara.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Strategies Tanzania, Jabiri Kigoda, amesema kampuni hiyo imejipanga kutoa huduma bora, za haraka na zinazoendana na mahitaji ya wateja.

Aidha, baadhi ya viongozi wa taasisi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo wamewahimiza wananchi kujiunga na huduma za bima ili kujikinga na athari za majanga yanayoweza kujitokeza, pamoja na kulinda mali na maisha yao.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbeya, Bw. Azizi Faki, ametoa onyo kali juu ya kuendelea kwa uharibifu wa vyanzo vya maji wilayani humo, akisema hali halisi ya uchafuzi na upungufu wa maji inaonekana wazi kutokana na shughuli za kibinadamu zisizozingatia sheria.

Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi wa chanzo cha maji cha Mtombalizi, kilichopo katika Kata za Utengule Usongwe na Nsalala, Bw. Faki alisema uchimbaji wa mchanga na mawe katikati ya mto pamoja na uharibifu wa kingo za maji umepelekea mto huo kupoteza mwelekeo wake wa asili, maji kuchafuka na kupungua kwa kiasi kikubwa.

Bw. Faki alisema licha ya kuwepo kwa maelekezo ya awali ya kulinda kingo za mito, kupanda miti na kuacha mita sitini kutoka kwenye chanzo cha maji bila shughuli za kibinadamu, hali bado ni mbaya kutokana na kuendelea kwa shughuli haramu, hali inayohatarisha vyanzo vya maji vinavyotegemewa na wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.

Alitoa wito kwa taasisi zote husika ikiwemo TFS, mamlaka za maji, mamlaka ya madini, Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Rukwa, pamoja na viongozi wa serikali za mitaa, kata na tarafa kushirikiana kikamilifu katika kulinda chanzo hicho. Alisisitiza kuwa jitihada za kutafuta kipato haziwezi kuwa sababu ya kuvunja sheria na kuharibu mazingira.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbeya, Mohamed Fakii, ametoa onyo dhidi ya uharibifu wa vyanzo vya maji unaotokana na ukataji miti ovyo na kilimo karibu na vyanzo vya maji.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa Chanzo cha Maji cha Mbawe, kijiji cha Mbawe, Fakii alisema kuwa shughuli za kibinadamu zinaendelea kuhatarisha uendelevu wa vyanzo vya maji licha ya kuwepo kwa maji kwa sasa kutokana na mvua. Alisisitiza kuwa ni marufuku kufanya shughuli zozote ndani ya mita 60 kutoka chanzo cha maji.

Aliwaagiza wananchi wote wanaolima au kufanya shughuli karibu na vyanzo hivyo kuondoka mara moja, huku akizitaka serikali za vijiji na kata kushirikiana kikamilifu katika ulinzi wa vyanzo vya maji na kutoa elimu kwa wananchi.

Ziara hiyo ilifanywa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbeya akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mheshimiwa Solomon Itunda, akiwa ameambatana na Kamati ya Usalama ya Wilaya.

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na Shirika la CARE wametoa mafunzo kwa wawezeshaji wa ngazi ya jamii kuhusu mabadiliko ya tabia nchi mkoani Mbeya kupitia Mradi wa Ustahimilivu Wake, Dunia Yetu unaotekelezwa katika vijiji 300 vya Mbeya, Njombe na Iringa.

Mafunzo hayo ya siku tatu yamefanyika kijiji cha Chimala, wilayani Mbarali, yakilenga kuwajengea wakulima na wafugaji uelewa wa masuala ya jinsia, utunzaji wa mazingira na mbinu za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.