Browsing: Video Mpya

Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya kwa kushirikiana na NHIF Mkoa wa Mbeya wamekutana na kundi la watu wenye ulemavu mkoani Mbeya kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kujiunga na Bima ya Afya kwa wote.

Akifungua kikao hicho Februari 25, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo Dkt. Godlove Mbwanji alisema lengo ni kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata uelewa wa bima hiyo, kwani ni miongoni mwa makundi maalumu yaliyopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita katika utekelezaji wa sheria ya Bima ya Afya kwa wote.

Msimamizi wa NHIF mkoa wa Mbeya, Bw. Nicolaus Mwangomo, alieleza kuwa washiriki walipatiwa elimu kuhusu utaratibu wa uchangiaji, faida na dhana ya bima hiyo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya Bima ya Afya kwa wote.

Kwa niaba ya washiriki, Bi. Rebecca Ramadhani alishukuru kwa elimu hiyo akisema itasaidia watu wenye ulemavu kukabiliana na changamoto za matibabu na kuboresha upatikanaji wa huduma za afya.

Miaka ya hivi karibuni, Mbeya limeendelea kushuhudia mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayochochewa na mazingira rafiki ya uwekezaji pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya kisasa. Miongoni mwa alama za maendeleo hayo ni ujenzi wa AH City Mall — jengo la kisasa lenye ngazi za umeme (escalator) ambalo limekuwa kivutio kikubwa kwa wakazi wa jiji na maeneo ya jirani. Watu wengi hufika si tu kwa shughuli za kibiashara, bali pia kwa matembezi na kupiga picha, wakivutiwa na hadhi yake ya kuwa jengo la kwanza katika Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini kuwa na mfumo huo wa kisasa wa ngazi za umeme.

Mtu anayedaiwa kuwa mwanafunzi wa Chuo cha Biashara (CBE) Kampasi ya Mbeya, Tido Kadaga (20), amekutwa amefariki dunia baada ya mwili wake kuonekana ukielea kwenye dimbwi la maji katika Mtaa wa Maili Tano, Kata ya Iganzo, Jijini Mbeya.
Kwa mujibu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania, walipokea taarifa kutoka kwa mashuhuda kuhusu mwili unaoelea majini na kufika eneo la tukio, kisha kuuopoa na kuupeleka Hospitali ya Rufaa Kanda Mbeya kwa uchunguzi zaidi.
Mrakibu Mwandamizi wa Zimamoto Mkoa wa Mbeya, Malumbo Ngata, amesema tukio hilo liliripotiwa majira ya mchana na baada ya uchunguzi wa awali kubainika marehemu ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza CBE.
Kwa upande wake, Mkuu wa chuo hicho, Dk Beny Mwenda, amesema wanangoja taarifa rasmi kutoka Jeshi la Polisi Tanzania kabla ya kutoa ufafanuzi zaidi.

ZAIDI ya kaya 200 zimepata madhara ya kukosa makazi baada ya nyumba zao kuezuliwa na nyingine kubomoka kufuatia mvua kubwa zilizoambatana na upepo mkali zinazoendelea kunyesha katika Nyanda za Juu Kusini.

Mbali na makazi kuharibika, vyakula na mavazi pia vimeathirika baada ya maji kujaa kwenye nyumba na mali nyingi kufunikwa na tope.

Uharibifu huo umeripotiwa katika kata sita, ambazo ni Iganzo, Isanga, Karobe, Iyunga, Nzovwe na Iwambi, wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Patrick Mwalunenge, aliyefika kujionea hali halisi ya wananchi walioathirika.

Baadhi ya wakazi wamesema chanzo kikubwa cha mafuriko hayo ni mifereji kuziba, hali iliyosababisha maji kuingia moja kwa moja kwenye makazi yao.

Licha ya uharibifu mkubwa wa mali na makazi, hakuna madhara ya kibinadamu yaliyoripotiwa hadi sasa.

Meneja Uhamasishaji Uwekezaji kutoka TISEZA, Daudi Riganda, amesema mamlaka hiyo inaendelea kuhamasisha uwekezaji ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za biashara nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutembelea mradi wa Babito Trading Company katika Mbeya, alisema uwekezaji huo unaomilikiwa kwa asilimia 100 na Watanzania umegharimu zaidi ya shilingi bilioni nane.

Alisema mradi huo ni chanzo cha mapato kwa jiji la Mbeya na pia kwa TRA, huku ukiwa mfano wa mafanikio ya uwekezaji wa ndani kutokana na mazingira mazuri ya biashara yaliyopo Tanzania.

Aidha, alibainisha kuwa motisha za uwekezaji, ikiwemo punguzo la kodi na unafuu wa ushuru kwa baadhi ya vifaa vilivyoagizwa kutoka China, zimechangia kupunguza gharama za mradi.