Browsing: Video Mpya

Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Uyole, Dkt. Tulia Ackson, ameunga mkono juhudi za wananchi wa Mtaa wa Bombambili, Kata ya Mwakibete mkoani Mbeya, kwa kuchangia mifuko 100 ya saruji na tripu 10 za mawe kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya zege iliyoanzishwa na wananchi kwa nguvu zao.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, vipande viwili vya barabara inayounganisha Kata za Iyela, Mwakibete na Mwasanga vinatarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi milioni 41, ambapo kipande kimoja kimegharimu zaidi ya milioni 23 na cha pili kinakadiriwa kugharimu zaidi ya milioni 18.

Diwani wa Kata ya Mwakibete, Lucas Mwampiki, alimshukuru Dkt. Tulia kwa kuendelea kuunga mkono maendeleo ya kata hiyo, huku akitaja pia msaada wake katika ujenzi wa nyumba inayotarajiwa kukabidhiwa Machi 7, 2026 katika Mtaa wa Itongo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Bombambili, Saidi George Kumbemba, alimpongeza Dkt. Tulia kwa kusaidia wananchi na wadau wanaojitolea kujenga barabara hiyo inayoelekea Makaburi ya Iyela, pamoja na kuendelea kuwatetea katika maendeleo ya miundombinu ya barabara.

Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya kwa kushirikiana na NHIF Mkoa wa Mbeya wamekutana na kundi la watu wenye ulemavu mkoani Mbeya kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kujiunga na Bima ya Afya kwa wote.

Akifungua kikao hicho Februari 25, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo Dkt. Godlove Mbwanji alisema lengo ni kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata uelewa wa bima hiyo, kwani ni miongoni mwa makundi maalumu yaliyopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita katika utekelezaji wa sheria ya Bima ya Afya kwa wote.

Msimamizi wa NHIF mkoa wa Mbeya, Bw. Nicolaus Mwangomo, alieleza kuwa washiriki walipatiwa elimu kuhusu utaratibu wa uchangiaji, faida na dhana ya bima hiyo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya Bima ya Afya kwa wote.

Kwa niaba ya washiriki, Bi. Rebecca Ramadhani alishukuru kwa elimu hiyo akisema itasaidia watu wenye ulemavu kukabiliana na changamoto za matibabu na kuboresha upatikanaji wa huduma za afya.

Miaka ya hivi karibuni, Mbeya limeendelea kushuhudia mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayochochewa na mazingira rafiki ya uwekezaji pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya kisasa. Miongoni mwa alama za maendeleo hayo ni ujenzi wa AH City Mall — jengo la kisasa lenye ngazi za umeme (escalator) ambalo limekuwa kivutio kikubwa kwa wakazi wa jiji na maeneo ya jirani. Watu wengi hufika si tu kwa shughuli za kibiashara, bali pia kwa matembezi na kupiga picha, wakivutiwa na hadhi yake ya kuwa jengo la kwanza katika Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini kuwa na mfumo huo wa kisasa wa ngazi za umeme.

Mtu anayedaiwa kuwa mwanafunzi wa Chuo cha Biashara (CBE) Kampasi ya Mbeya, Tido Kadaga (20), amekutwa amefariki dunia baada ya mwili wake kuonekana ukielea kwenye dimbwi la maji katika Mtaa wa Maili Tano, Kata ya Iganzo, Jijini Mbeya.
Kwa mujibu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania, walipokea taarifa kutoka kwa mashuhuda kuhusu mwili unaoelea majini na kufika eneo la tukio, kisha kuuopoa na kuupeleka Hospitali ya Rufaa Kanda Mbeya kwa uchunguzi zaidi.
Mrakibu Mwandamizi wa Zimamoto Mkoa wa Mbeya, Malumbo Ngata, amesema tukio hilo liliripotiwa majira ya mchana na baada ya uchunguzi wa awali kubainika marehemu ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza CBE.
Kwa upande wake, Mkuu wa chuo hicho, Dk Beny Mwenda, amesema wanangoja taarifa rasmi kutoka Jeshi la Polisi Tanzania kabla ya kutoa ufafanuzi zaidi.