Browsing: Video Mpya

Maadhimisho ya Siku ya Msichana katika Chuo Kikuu cha Mzumbe, Ndaki ya Mbeya, yalifanyika kwa mafanikio tarehe 10 Mei 2025. Hafla hii ilihudhuriwa na Mgeni Rasmi Mheshimiwa Maryprisca Mahundi, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya na Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Maryprisca Women Empowerment Foundation (MWEF).

Katika hotuba yake, Mh. Mahundi aliwasihi wasichana wa chuo kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuathiri mustakabali wao, akisisitiza umuhimu wa elimu kama nyenzo ya kujikomboa kiuchumi na kijamii. Rasi wa Ndaki ya Mbeya, Prof. Henry Mollel, alishiriki pia na kupongeza waandaaji, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza maadhimisho haya kila mwaka.

Hafla hiyo ilijumuisha vipindi vya elimu, burudani, na majadiliano kuhusu nafasi ya msichana katika jamii. Mh. Mahundi aliahidi kuchangia shilingi milioni 5 kwa ajili ya ujenzi wa hosteli ya wanafunzi wa kike Ndaki ya Mbeya.

Siku hii huadhimishwa kila mwaka na Jumuiya ya Wasichana wa Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Mbeya kwa kushirikiana na Serikali ya Wanafunzi (MUSO).

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb), amempongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, kwa uongozi wake wa mfano unaoleta mageuzi chanya kupitia Mbeya Tulia Marathon.

Akizungumza Mei 10, 2025 katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya, mara baada ya kushiriki mbio fupi za Tulia Marathon, Mhe. Mahundi alisema kuwa mashindano hayo si tu ni burudani ya michezo bali pia ni jukwaa la kugusa maisha ya Watanzania wengi kupitia uboreshaji wa huduma za afya, elimu na kusaidia makundi yenye uhitaji.

“Spika Tulia si kiongozi tu wa kitaifa, bali ni dira ya matumaini kwa jamii. Kupitia Mbeya Tulia Marathon ameonyesha kuwa michezo ni daraja la maendeleo,” alisisitiza Mhe. Mahundi.

Mashindano haya yameendelea kuthibitisha kuwa michezo inaweza kuwa chachu ya mshikamano, afya bora, na maendeleo endelevu kwa taifa.